Kupunguza Vifo vya Watoto
Kiwango cha chanjo zote kwa watoto chini ya umri wa mwaka mmoja kimeongezeka kutoka asilimia 91 (mwaka 2005) hadi asilimia 93 (mwaka 2006) . Katika kupunguza vifo vya watoto, halmashauri zote zinatekeleza mpango wa ”Intergrated Management of Childhood illness” ambao unahusika na kutibu magonjwa ya malaria, kichomi, kuharisha, surua, upungufu wa damu na utapiamulo. Vifo vya watoto wa umri chini ya miaka mitano vimepungua kutoka 150/1000 mwaka 2000 hadi 112/2000 mwaka 2004 (Dermographic Health Survey of 2004)
Kupunguza Vifo vya akina mama vinavyotokana na Uzazi
Kiwango cha wajawazito waliojifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma za afya kimeongezeka kutoka asilimia 53.8 mwaka 2005 hadi asilimia 57 mwaka 2006. Katika kupunguza vifo vya akina mama vinavyotokana na uzazi, halmashauri zote zinatekeleza mpango wa Huduma za dharura kwa wajawazito. Vifo vya akina mama vinavyotokana na uzazi vimepungua kutoka 135/100,000 mwaka 2005 hadi 118/100,000 mwaka 2006.
Kudhibiti ugonjwa wa Malaria
Kiwango cha wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano wanaotumia vyandarua viuatilifu kimeongezeka kutoka asilimia 35 mwaka 2003 hadi asilimia 68 mwaka 2006. Kiwango cha vifo vya watoto chini ya umri wa miaka mitano kutokana na ugonjwa wa Malaria kimepungua kutoka asilimia 22.8 mwaka 2002 hadi asilimia 13 mwaka 2006. Aidha Mkoa haukupata mlipuko wa Malaria mwaka 2007 kama ilivyokuwa inatokea miaka ya 1998 hadi 2006.
Kudhibiti ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma.
Vituo vya tiba vinavyotumia ”Direct Observed Treatments” kwa ugonjwa wa Kifua Kikuu vimeongezeka kutoka 15 mwaka 2001 hadi 68 mwaka 2006. Idadi ya vituo vya tiba vinavyotumia ”Multi Drug Therapy” kwa ugonjwa wa Ukoma vimeongezeka kutoka 40 mwaka 2003 hadi 75 mwaka 2006.
Kudhibiti UKIMWI.
Mkoa umefikisha elimu kuhusu ugonjwa wa UKIMWI kwa wanainchi na kiwango cha ”HIV/AIDS awareness” kimeongezeka kutoka asilimia 75 mwaka 2004 hadi asilimia 95 mwaka 2006. Mkoa umeweza kutoa dawa za kurefusha maisha ya watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI katika hospitali nane. Kuanzia Mei 2005 hadi Desemba 2006 , jumla ya wagonjwa 2,619 walianzishiwa madawa kati ya watu 5,183 waliosajiliwa. Mkoa una vituo 18 vinavyotoa huduma za kuzuia maambukizo ya Virusi vya UKIMWI kutoka kwa mama mjamzito kwenda kwa mtoto (PMTCT) . Mkoa pia una vituo 43 vinavyotoa huduma za ushauri nasaha na upimaji wa hiari wa viruzi vya UKIMWI.
Utafiti uliofanywa na TACAIDS mwaka 2004 uligundua kuwa kasi ya maambukizo ya Virusi vya UKIMWI (HIV Prevalence) ilikuwa asilimia 3.7 ukilinganisha ya kitaifa ambayo ni asilimia 7. Mkoa uliendesha kampeni ya Taifa ya upimaji wa Virusi vya UKIMWI kwa hiari kuanzia tarehe 22 Septemba 2007 hadi 26 Novemba, 2007. Matokeo ni kuwa wanainchi 172,768 kati ya walengwa 253,988 walipimwa sawa na asilimia 68. Aidha watu 6,514 kati ya watu 172,768 waliopimwa walikutwa na Virusi vya UKIMWI (HIV POSITIVE) sawa na asilimia 3.8.
Maboresho katika Sekta ya afya
Lengo la mabadiliko yanayofanyika katika Sekta ya afya ni kuboresha huduma na kusambaza huduma za afya katika maeneo ya vijijini ambapo asilimia 80 ya wanainchi wanaishi. Katika kutoa madaraka zaidi kwa halmashauri juu ya uendeshaji wa huduma za afya, Bodi za afya (Council Health Service Boards) na kamati za vituo vya afya na Zahanati zilianzishwa na kuimarishwa. Mpango wa ”Indent System” umeanzishwa katika halmashauri zote ili kuhakikisha kwamba dawa na vifaa muhimu vinapatikana katika vituo vyote vya kutolea huduma za afya. Katika kutafuta vyanzo vipya vya fedha za kuendeshea huduma za afya Halmashauri ya Karagwe imeanzisha mfuko wa afya ya Jamii (Community Health Fund) . Aidha halmashauri zingine ziko kwenye hatua mbali mbali za kuanzisha mfuko huo wa afya ya jamii.
CHANGAMOTO
Mkoa unakabiliwa na matatizo yanayoathiri utoaji bora afya.
Mkoa una upungufu wa watumishi wenye stadi na ujuzi unaotakiwa
Mkoa bado una upungufu wa zahanati 448, Vituo vya afya 130, na hospitali 7. (Jedwali Na.10).
Mkoa una upungufu wa vitendea kazi (Jedwali Na. 6).
MIKAKATI
Sera ya Taifa ya afya ni kusogeza huduma za afya karibu na wananchi. Kwa hiyo matarajio ya Mkoa ni kutekeleza mpango wa maendeleo ya afya (MMAM) .
Katika kutekeleza sera hiyo mkoa utakamilisha mpango wa ujenzi wa zahanati katika kila kijiji na Kituo cha afya katika kila kata.
Katika mwaka 2007/2008 mkoa unatarajia kuajiri wataalamu ili kukidhi mahitaji ya zahanati na vituo vya afya vilivyopo.
Ujenzi rasmi wa zahanati na vituo vya afya vipya utaanza mwaka 2008/2009.
Katika mpango huu wa MMAM tutatumia dhana ya ushirikishwaji wa wananchi kama ilivyotumika katika mpango wa maendeleo wa Elimu ya msingi na Sekondari. |