JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA - OFISI YA MKUU WA MKOA KAGERA
     
 
     
 
 
     
 
Ardhi [ Upimaji ] [ Ramani ] [ Nyumbani ] au
 

KILIMO CHA UMWAGILIAJI MKOA KAGERA

UTANGULIZI

Mabadiliko ya tabianchi.

Dunia imekuwa na mabadiliko makubwa ya tabianchi yanayosababisha uhaba wa mvua na hatimaye kuleta upungufu mkubwa wa uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara.

Hali ya mabadiliko ya tabianchi imefanya majira ya mvua katika Mkoa wa Kagera kubadilika msimu wa mvua za vuli kuchelewa kuanza ambapo sasa mvua zinaanza kunyesha Novemba badala ya mwezi Septemba wakati mvua za masika zinaanza kunyesha mwezi Aprili badala ya mwezi Februari hadi Juni.

 

Sera na Maelekezo ya Serikali

Hali hii imefanya Serikali kuanzisha Sera ya Umwagiliaji ya mwaka 2010 kwa lengo la kuinua Kilimo cha Umwagiliaji na kukifanya kilimo hicho kisitegemee mvua pekee.

Pamoja na sera ya umwagiliaji yapo maelekezo yanayosisitiza Kilimo cha Umwagiliaji:

•  Mpango wa Serikali wa Maendeleo wa miaka mitano kuanzia 2011 hadi 2015.

•  Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010 ambayo katika ibara ya 34 kifungu kidogo cha (a) hadi (f) imesisitizwa kutumia kilimo cha umwagiliaji kwaajili ya kukuza uchumi wa taifa na wananchi katika kipindi hiki kwa kuongeza uhakika wa upatikanaji wa chakula nchini.

•  Mpango mkakati wa miaka mitano wa Sekretariet ya Mkoa wa Kagera ambao ulisisitiza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara utokane na Kilimo cha Umwagiliaji

 

Aina mbalimbali za Umwagiliaji

Umwagiliaji unaweza kufanywa kwa kutumia njia mbalimbali ambazo ni pamoja na:

1. Njia ya mafuriko (Surface Irrigation).

2. Njia ya mabomba (Sub surface Irrigation).

3. Njia ya mtawanyo (Sprinkler Irrigation).

4. Njia ya matone (Drip Irrigation).

 

Mikakati inayotumika

Mkoa kwa kushirikiana na Halmashauri za Wilaya pamoja na wadau wengine wa maendeleo umejiwekea mikakati mbalimbali ya utekelezaji.

Mikakati hiyo ni pamoja na:

•  Kuhamasisha umma na sekta binafsi katika Kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuhakikisha kwamba mifumo ya umwagiliaji (Inayoanzishwa na itakayoanzishwa) inazingatia sheria na taratibu za nchi.

•  Kuhamasisha matumizi bora ya rasilimali maji katika mifumo ya Kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuhakikisha kwamba Maendeleo ya Kilimo cha umwagiliaji yanazingatia masuala ya kiufundi, kiuchumi, kijamii na kimazingira.

•  Kuhakikisha kwamba rasilimali maji ya umwagiliaji yanatumika kikamilifu kwa kiwango cha juu kwa kuzingatia tija.

•  Kuhakikisha kwamba miundo ya maendeleo ya kilimo cha umwagiliaji(Irrigation development models) inatumika kuzalisha mazao yenye tija kulingana na mahitaji ya soko.

•  Kuhuisha masuala mtambuka kama vile jinsia, ukimwi, mazingira, afya, ardhi na maji katika maendeleo ya Kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuendelea kutekeleza Kilimo cha umwagiliaji kupitia programu ya maendeleo ya Sekta ya Kilimo (ASDP) kwa kuongeza eneo lenye miundo mbinu ya umwagiliaji kutoka hekta 19,414 za Juni 2011 hadi hekta 50,000 ifikapo mwaka 2015. Sekta binafsi itashirikishwa katika uendelezaji na uwekezaji kwenye kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuzihimiza Halmashauri kukamilisha kutunga sheria ndogo za umwagiliaji.

•  Kujenga na kukarabati miundombinu ya umwagiliaji ya wakulima wadogo na wakati ili kuongeza uzalishaji na ufanisi wa matumizi ya maji.

•  Kujenga na kukarabati mabwawa ya kuvuna na kuhifadhi maji ya mvua na mito kwa ajili ya umwagiliaji kwa kila Halmashauri ya wilaya.

•  Kujenga uwezo wa Taasisi zinazohusika na umwagiliaji katika ngazi ya Halmashauri za wilaya na wakulima katika usimamizi na uendeshaji endelevu wa miradi ya umwagiliaji.

 
HALI HALISI YA UMWAGILIAJI

Wilaya

Eneo linalofaa kwa umwagiliaji (Ha)

Eneo linalotumika kwa umwagiliaji(Ha)

Asilimia ya matumizi(%)

Bukoba

1,300

10

0.769

Muleba

5,895

320

5.43

Missenyi

20,463

15,564

76.05

Ngara

5,000

3,000

60

Biharamulo

500

0

0

Karagwe

960

120

12.5

Chato

10,710

400

3.73

JUMLA

44,828

19,414

43.3

 

 
 
 

 

 

 

 
 
 
 
 

 

 
 
 
 
 

Eng. Msafiri E. Magungu--Mhandisi Kilimo

 

Maeneo yanayofaa kwa Kilimo cha Umwagiliaji

 

Hapo juu ni takwimu za maeneo yanayofaa kwa kilimo cha umwagiliaji pamoja maeneo yanayolimwa kwa sasa Mkoani Kagera hadi kufikia Julai, 2011.

NB: Maeneo hayo yanayotumika kwa umwagiliaji ni yale ya umwagiliaji mkubwa kama vile Kagera Sugar na Umwagiliaji mdogo kwa maeneo mengine yaliyobaki (isipokuwa Kagera Sugar).

 

 

 

Miradi ya Umwagiliaji inayoendelea kutekelezwa na fedha zilizotengwa kwaajili utekelezaji katika Halmashauri za Mkoa wa Kagera kuanzia mwaka 2009/10 hadi 2011/12.

Katika kuhakikisha maeneo hayo yaliyoanishwa hapo juu yanatumika ipasavyo kwa Kilimo cha Umwagiliaji, Serikali kupitia Mpango wa Kuendeleza Sekta ya Kilimo nchini(ASDP) kwa kushirikisha wadau wa maendeleo kama vile Benki ya Maendeleo ya Afrika(AfDB) imeweza kuleta fedha ili kutekeleza uanzishwaji wa Miradi ya Umwagiliaji katika maeneo mbalimbali ikiwa inamilikiwa na Serikali pamoja na Wananchi wa maeneo husika.

Na hivi sasa Miradi mingi iliyopata fedha hizo kutoka Serikalini ipo katika hatua za awali za utekelezaji ukiachilia mbali Miradi ya Buyaga na Buhangaza iliyopo Wilayani Muleba ambayo ipo katika hatua za mwisho kukamilika ingawaje Mradi wa Buhangaza ulisumbua kidogo katika utekelezaji wake kutokana na matatizo yaliyompata Mkandarasi wa Mradi huo katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi(Climatical change) na matatizo ya kijiolojia(Geological problems) katika eneo la Mradi ila kwa sasa unaendelea vizuri.

CHANGAMOTO

Changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa mikakati ya kilimo cha umwagiliaji kwa msimu wa mwaka 2010/2011:

•  Bajeti ndogo ya uwekezaji katika kilimo cha umwagiliaji.

•  Uwezo na ushiriki mdogo wa taasisi binafsi katika maendeleo ya kilimo cha umwagiliaji.

•  Ujuzi mdogo kwa wakulima kuhusu kilimo cha umwagiliaji.

•  Uwezo mdogo wa Halmashauri za wilaya katika uwekezaji na utekelezaji wa Kilimo cha umwagiliaji.

•  Utumiaji mdogo wa maji (insufficient water use) unaosababisha ukosefu wa tija katika sekta ya kilimo cha umwagiliaji.

•  Ukosefu wa mifumo bora ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji.

•  Ukosefu wa vihifadhi bora vya maji (Water storage facilities) kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya kilimo cha umwagiliaji.

•  Kukauka kwa vyanzo vya maji kunakosababishwa na mabadiliko ya tabianchi.

•  Upungufu wa wataalamu wa umwagiliaji katika Halmashauri za wilaya.

 

NAMNA YA KUKABILIANA NA CHANGAMOTO.

Katika msimu wa Kilimo wa 2010/2011, Mkoa ulijiwekea lengo la kuanzisha Miradi ya Umwagiliaji katika maeneo mbalimbali yanayofaa kwa Kilimo cha Umwagiliaji katika Halmashauri za Wilaya ambapo kutokana na upembuzi yakinifu uliofanywa na wataalamu wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kupitia Ofisi ya Umwagiliaji Kanda, inakadiriwa ni hekta 44,828 ndizo zinazofaa kwa Kilimo cha Umwagiliaji Mkoani Kagera.

Pamoja na uanzishwaji wa Miradi ya Umwagiliaji, Halmashauri ya Missenyi imeanza zoezi la ukarabati wa miundombinu ya umwagiliaji katika Mradi wa Umwagiliaji Nkenge wenye hekta 1300 ambapo sehemu moja ya Mradi yenye hekta 200 imekabidhiwa kwa Jeshi la Magereza na sehemu nyingine yenye hekta 1100 imekabidhiwa kwa wakazi wa maeneo hayo pamoja na watumishi wanaopenda kuendeleza shughuli za Kilimo ili kuhamasisha kilimo katika maeneo ya Mradi huo.

Ujenzi na ukarabati wa mabwawa ya kuvuna na kuhifadhi maji ya mvua na mito kwa ajili ya umwagiliaji unakwenda sambamba na zoezi la uanzishwaji wa Miradi ya Kilimo katika maeneo ya Miradi ya Umwagiliaji katika Halmashauri za Wilaya.

Katika kukabiliana na changamoto zilizopo, Serikali Mkoani Kagera imepanga kufanya yafuatayo ili kuendeleza kilimo cha umwagiliaji katika msimu wa mwaka 2011/12:

•  Kuzishauri Halmashauri za Wilaya kutenga bajeti ya kutosha katika sekta ya umwagiliaji.

•  Kuhamasisha taasisi binafsi ili ziweze kushiriki vema katika kuendeleza sekta ya kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuwawezesha wakulima mbinu mpya na bora zitakazosaidia kuendeleza kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuhamasisha matumizi bora na endelevu ya rasilimali maji kwaajili ya kufanikisha kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuandaa mifumo bora, endelevu na yenye tija kwa ajili ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuzihimiza Halmashauri kuandaa mipango bora na matumizi bora ya ardhi kwa sekta ya umwagiliaji.

•  Kusimamia ujenzi wa vihifadhi bora vya maji (Water storage facilities) vitakavyosaidia kuendeleza kilimo cha umwagiliaji.

•  Kuhamasisha na kuendeleza juhudi za utunzaji wa mazingira hasa maeneo yazungukayo miradi ya umwagiliaji ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi (Climatical Change).

•  Kuzishauri Halmashauri za wilaya ili zitenge bajeti za kuajiri wataalamu wa umwagiliaji.

 

 
 
 
 
 

 

 
 
 
 
     
     
 
     
Copyright © 2008 - Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera, BUKOBA, TEL: 028 - 2220215/17, FAX: 028-2752184