Ili kuratibu shughuli yoyote ndani ya nchi/mkoa mfanyabiashara/mjasiriamali atatakiwa kutimiza masharti yafuatayo.
Awe na sehemu maalum ya kufanyia biashara.
Awe na Namba ya utambulisho wa Mlipa Kodi (TIN-Tax Identification Number) ambayo hutolewa na Mamlaka ya Mapato Tanzania.
Kwa biashara zenye udhibiti mfano, usafirishaji, vituo vya mafuta, shule n.k ni lazima awe na leseni ya Mamlaka husika kama vile SUMATRA, EWURA, n.k.
Awe na leseni ya biashara husika inayotolewa na Halmashauri husika.
Cheti cha usajili wa kampuni (Company Certificate of Registration) kama ni kampuni au cheti cha usajili wa jina la biashara (Business Name Registration Certificate) husika kutoka BRELA.
Taratibu za biashara ya nje
Ili kufanya biashara nje ya nchi mfanyabiashara anashauriwa kukamilisha au kuandaa vitu vifuatavyo:-
Leseni ya biashara ya kununua na kuuza nje (Import & Export License) ambayo hutolewa na Wizara ya Viwanda na Biashara kupitia Ofisi ya Biashara Mkoa.
Vibali vya biashara husika, mfano vibali vy akusafirisha mazao nje ya nchii.
Chati cha Uasili (Certificate of Origin) kama kwa nchi wanachama wa jumuiya ya Afrika Mashariki. Hii humsaidia Mfanyabiashara kuondokana na kodi ya kuingiza bidhaa (Import duty 25%) ndani ya nchi husika kutoka katika nchi wananchama, na badala yake atatakiwa kulipia kodi ya ya ongezeko la thamani pekee.
Cheti cha uanachama wa Chemba ya Wafanyabiashara wenye viwanda na biashara (TCCIA Membership Certificate.
Cheti cha usajili wa kampuni(Company Certificate of Registration) kama ni kampuni au cheti cha usajili wa jina la biashara (Business Name Registration Certificate) husika kutoka BRELA.
Cheti cha ubora wa bidhaa kutoka TFDA-Mamlaka ya chakula na dawa au Shirika la Viwango Tanzania TBS.
Taratibu za biashara zenye uthibiti maalum
Biashara zenye udhibiti zinazozungumziwa hapa ni pamoja na biashara za vituo vya mafuta ya dizeli, petrol, mafuta ya taa, biashara ya usafirishaji abiria kwa magari/mabasi, usafiri wa majini kwa meli na boti, biashara za mitandao ya mawasiliano ya simu, radio, televisheni, usafiri wa anga, biashara za madawa ya binadamu na mifugo, n.k. Leseni za biashara hizi hutolewa mara tu baada ya mamlaka husika kuwa imejiridhisha na masuala ya kitaalam na kutoa kibali/leseni ya mamlaka hiyo ndiyo Ofisi ya biashara inaweza kutoa leseni ya biashara. Changamoto iliyopo ni kuwa mamlaka zilizo nyingi bado hazijaimarishwa na kuwa na Ofisi katika kila makao makuu ya mikoa, mfano EWURA, BRELA n.k
Bei za Bidhaa
Katika kipindi cha nyuma serikali iliwahi kuunda chombo cha kudhibiti bei za bidhaa zote, chombo kilifahamika kama tume ya bei (Price commission). Hata hivyo, serikali ilipojitoa katika masuala ya kufanya biashara na tangu kuanzishwa kwa soko huria bei za bidhaa mbalimbali ambazo hazina mamlaka maalum za udhibiti zimekuwa zikiendeshwa/kuamuriwa na nguvu ya soko pamoja na ushindani wa soko.
Utoaji wa leseni za Biashara
Kuna makundi mawili ya leseni za biashara kwa mujibu wa sheria za leseni ya leseni za biashara namba 25 ya mwaka 1972 iliyofanyiwa maboresho mwaka 1982. Makundi hayo ni: i) kundi la leseni zinazotolewa na mamlaka za serikali za mitaa (Halmashauri za Wilaya na Manispaa) ii) kundi la pili ni leseni zinazotolewa na Wizara ya Viwanda na Bisahara mfano leseni za kufungua na kuendesha Klabu za Muziki za Usiku (Night Clubs) na leseni za kununua na kuuza nje ya nchi (Import and Export License).
Masharti ya kuomba leseni za biashara kwa makundi yote mawili ni kama ifuatavyo:-
Cheti cha usajili wa Kampuni au jina la biashara (Certificate of registration/incorporation)
Kama ni kampuni “memorandum and article of Association''.
Cheti cha urai (Passport ya Tanzania) au cheti cha kuzaliwa au hati ya kiapo (affidavit).
Mkataba wa jengo analofanyia biashara husika au hati ya umiliki endapo jengo ni lake.
Hati ya kujiandikisha kama mlipa kodi (TIN)
Endapo wana hisa wa kampuni wapo nje ya nchi maombi yaambatane na hati ya kiwakili.
Hatua za kupata leseni ya biashara
Pamoja na kukamilisha masharti hayo, ili kupata leseni siku za nyuma mwombaji alitakiwa kupitisha fomu ya maombi iliyojazwa katika Ofisi za mipango miji, ofisi za afya na hatimaye Ofisi za biashara tayari kwa kupata leseni husika baada ya kuwa wote wamekagua maeneo yao kitaalam na kujiridhisha. Hatua hiyo ilionekana kuwa na urasimu mwingi na kufanya ucheleweshaji wa kutoa leseni hatimaye biashara nyingi zilikuwa zikichelewa kuanzishwa. Ikiwa ni hatua za kurahisisha uanzishaji na uendeshaji wa biashara, sharti la kupitisha fomu ya maombi ya leseni katika ofisi za afya na mipango miji limeondolewa. Aidha, baada ya kukamilisha taratibu zote pamoja na nyaraka zote zinazohusika mwombaji itamchukua muda wa siku moja hadi tatu tu kuwa amepata leseni yake kutoka katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa alipoombea leseni yake.
Ada za leseni
Kwa kipindi kirefu ada za leseni kwa mujibu wa sheria zilikuwa kati ya shilingi 10,000 hadi 500,000 kutokana na aina ya leseni, eneo la biashara na aina ya biashara inayoombewa leseni. Wakati fulani ada hizo ziliondolewa na kwa kipindi kirefu leseni zilikuwa zikitolewa bure ili kurahisisha watu wengi zaidi kuhamasika na kuanzisha biashara ili kuiongezea serikali mapato kwa kuwa na vyanzo vingi vya mapato.
Hata hivyo serikali katika bunge la bajeti la mwaka 2011/2012 imerudisha utaratibu wa ada za leseni za biashara na utaratibu huu utaanza kutumika rasmi Januari Mosi, 2012. Umetolewa muda wa kutosha kuzipa Halmashauri za Wilaya muda wa kujiandaa na kuweka miundombinu vizuri ili zoezi hili litakapoanza liende kwa kasi inayotarajiwa na kuleta matunda kwa serikali za mitaa ili kupunguza utegemezi kutoka serikali kuu.
Hivyo ni muhimu kwa kila mfanyabiashara kuhamasika na kusajili biashara yake ikiwa ni pamoja na kuikatia leseni ya biashara husika ili kufanya biashara kwa haki, uhuru na amani na kuchangia kikamilifu ujenzi na uimarishaji wa uchumi wa Mkoa wa Kagera na Taifa kwa ujumla.
Usajili wa shughuli za biashara
Kwa mujibu wa Sheria ya Usajili wa Shughuli za Biashara Namba 14 ya mwaka 2007 Registration Act No 14 of 2007) ya biashara inatakiwa kusajiliwa na kupewa chaeti cha kudumu ili kutambulika kuwa ni biashara rasmi. Usajili wa jina la biashara umekuwa ukifanywa na Wakala wa Usajili wa Makampuni na Majina ya Biashara Tanzania ambaye ni BRELA. Wakala huyu ndiye mtekelezaji Mkuu wa Sheria ya BARA na 14 ya mwaka 2007, aidha BRELA iko chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara sambamba na taasisi za SIDO, TBS na Wakala wa Vipimo (WMA-Weights and Measure Agency).
Ada ya Usajili wa Jina la Biashara (Business Name Registrtion Fee)
Ada ya usajili wa Jina la Biashara ni shilingi za Kitanzania elfu sita tu 6,000/=. Kuna fomu maalum za kujaza ili kuweza kujisajili kama biasharar ya mtu binafsi au kama biashara ya ubia (watu zaidi ya mmoja mpaka 20). Fomu za maombi ya usajili wa Jina la Biashara zinapatikana katika tovuti ya Mkoa wa Kagera, na kwa maelezo zaidi ya msaada namna ya kusajili jina la biashara wasiliana na Ofisi ya Biashara Mkoa wa Kagera.
Soko la Afrika Mashariki
Hili ni soko la pamoja linalojumuisha nchi za Afrika Mashariki ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi. Ni soko kubwa sana lenye zaidi ya watu zaidi ya milioni 120 linaloruhusu mwingiliano wa bidhaa, watu, fedha, mitaji, huduma pamoja na masula ya forodha. Kuna fursa nyingi zinazotokana na soko la pamoja la Afrika Mashariki, ikiwa ni pamoja na idadi kubwa ya watu wanaohitaji bidhaa mbalimbali kutoka katika nchi wananchama mfano; mazao ya chakula kama mahindi, mchele, mihogo, viazi, sukari, nguo, magodoro, viatu, rasilimali watu, mitaji. Aidha Mkoa wa Kagera unayo fursa ya kipekee ya kijiografia kwa kuwa umepakana karibu na nchi zote za Afrika ya mashariki. Ni dhahili kuwa Wananchi wa Mkoa wa Kagera wanapaswa kuelewa umuhimu wa shirikisho hili kwa kuanza kuzalisha kwa wingi bidhaa na mazao mengi zaidi kwa ajili kuhudumia na kuuza kwa wingi katika nchi wananchama.
Vikwazo na Changamoto za biashara mipakani
Uzalishaji duni wa mazao na bidhaa mbalimbali hivyo kupelekea kutokidhi mahitaji ya soko la ndani na nje.
Ukosefu wa masoko ya mipakani.
Ukosefu wa maghala maeneo ya mipakani kwa ajili ya kuhifadhia bidhaa/mazao.
Maeneo ya mipakani hayana taasisi za fedha na benki kwa ajili ya kurahisisha huduma za kifedha mipakani.
Biashara nyingi maeneo ya mipakani zipo upande wa nchi za jirani.
Maeneo ya mipaka ya Tanzania hayana nishati ya umeme.
Wafanyabiashara wengi wana elimu ndogo ya biashara ya kimataifa.
|