Shughuli ya udhibiti wa gugu maji katika ziwa Victoria pamoja na mito/mabwawa iliendelea kufanyika kwa kutumia njia husishi (Biological control). Katika njia hii husishi wadudu aina ya MBAWA KAVU (Water Hyacirth weevils) ndiyo hutumika kuangamiza gugu maji. Wadudu hawa ni Rafiki wa mazingira kwani hawana madhara yoyote kwa viumbe wengine.
Utafiti unaendelea kufanyika kuhusu njia ya kudhibiti gugu maji ndani ya mto Kagera na mito mingine maana mdudu wa MBAWA KAVU hawezi kufanya kazi yake vizuri kwenye mito kutokana na kasi ya maji. Wataalamu wanaangalia uwezekano wa kutumia mdudu mbadala aina ya MITES.
Hifadhi ya Mazingira ya Miji na Utupaji Taka
Katika kuadhimisha siku ya mazingira Duniani mwaka huu, kila Wilaya ilielekezwa kuandaa Program ya maadhimisho haya. Mingoni mwa shughuli zilizoainishwa katika program za Wilaya zote ni kusafisha mitaro, kufanya usafi katika maeneo ya makazi, maeneo ya biashara (Masoko) pamoja na kuhimiza utumiaji wa mashimo au vyombo vya kutupia taka za majumbani.
Utekelezaji wa program hizi za Wilaya bado ni hafifu isipokuwa kwa Wilaya ya Karagwe ambao wametekeleza Program yao kwa zaidi ya asilimia 90. Ziara ya ujumbe wa Ofisi ya Makamu wa Rais
Katika kipindi hiki kuanzia tarehe 26 Julai hadi 30 Julai, 2009 Mkoa ulitembelewa na ujumbe kutoka ofisi ya Makamu wa Rais kwa ajili ya kukagua na kuona hali halisi ya mazingira. Ujumbe wa Ofisi ya Makamu wa Rais uliongozwa na Katibu Mkuu (OMR) Bibi Ruth Mollel. Ujumbe uliweza kutembelea na kukagua shughuli za Hifadhi ya mazingira katika Wilaya za Bukoba Vijijini, Muleba, Missenyi na Manispaa ya Bukoba.
Baada ya ziara hiyo ya siku nne, Ofisi ya Makamu wa Rais iliuandikia Mkoa barua ya Pongezi kutokana na jitihada zinazofanywa na viongozi pamoja na Wananchi katika kuhifadhi Mazingira. Aidha, Mkoa umeelekezwa kuendelea kuhamasisha jamii katika upandaji wa miti pamoja na kuepuka uchomaji moto ovyo.
Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi
Kauli Mbiu ya maadhimisho ya siku ya Mazingira Duniani Mwaka 2009 ilikuwa ni “ Dunia inakuhitaji; Tuungane kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi”. Muhtadhari wa kauli Mbiu hii ni kuhimiza uwajibikaji wa kila mtu na kila sekta katika Kupambana na kujiweka tayari kukabiliana na mabadiliko ya Tabia nchi kwa kuhifadhi mazingira.
Chanzo kikuu cha mabadiliko ya Tabianchi (climate change) ni kuongezeka kwa joto Duniani. Kuongezeka kwa joto kunasabishwa na gesijoto ( green - house gases ) kwa kiwango kikubwa kuliko kiasi halisi kinachohitajika kuwezesha uhai na mifumo ya Dunia kuwa katika hali yake ya asili. Katika mazingira yetu, gesijoto ni Carbon-Dioxide, Methani na nyinginezo ambazo zinatokana na shughuli za kila siku za Mwanadamu, kwa mfano viwanda, vyombo vya usafirishaji, ukataji misitu, uchomaji moto ovyo pamoja na kilimo kisicho endelevu.
Athari za mabadiliko ya Tabianchi zinazoweza kutukabili tusipochukua tahadhari ni:-
Kubadilika na kutotabirika kwa misimu ya mvua.
Kushuka au kupungua kwa mavuno katika mashamba.
Kuongezeka kwa majanga ya mafuriko/ukame
Kupungua kwa theluji katika vilele vya milima (mfano mlima Kilimanjaro) kwa kasi kubwa.
Kushuka au kupungua kwa kina cha maji katika mito na maziwa.
Kuenea kwa maradhi ya Malaria hata kwenye maeneo yenye baridi ya hali ya juu kama vile Bukoba, Ngara na Karagwe
Ili kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi, sote kwa pamoja tunasisitizwa kuendelea kuchukua hatua za dhati, kwa kutumia nyadhifa zetu, kuzuia uharibifu wa mazingira na kuboresha palipo haribika. Tayari Serikali imetuandalia “ Silaha ” tatu za kupambana na adui yetu huyu, nazo si nyingine bali ni:-
Sheria ya Usimamizi wa mazingira ya mwaka 2004
Mpango wa Taifa wa kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (2006)
Mkakati wa Taifa wa Kuhifadhi Mazingira ya Ardhi na vyanzo vya Maji (2006).
|