Malengo ya Kilimo Msimu 2009/2010
Katika msimu wa kilimo 2009/2010 Mkoa umejiwekea lengo la kulima na kutunza jumla ya hekta 738,300 za mazao mbalimbali ya chakula zilizotarajiwa kuzalisha jumla ya tani 1,369,800 za ndizi, tani 355,700 za nafaka, tani 130,300 za mikunde na tani 995,600 za mazao ya mizizi.
Aidha, mkoa umelenga kulima na kutunza jumla ya hekta 105,000 za mazao mbalimbali ya biashara zilizotarajiwa kuzalisha jumla ya tani 40,000 za kahawa, tani 220 za tumbaku, tani 16,000 za pamba mbegu, tani 4,500 za majani mabichi ya Chai.
Mahitaji na Upatikanaji wa Chakula Msimu 2009/2010
Inakadiriwa kuwa mwaka 2010 idadi ya wakazi wa mkoa wa Kagera itafikia 2,563,800 (maoteo). Mahitaji ya chakula kwa wakazi wa mkoa huu kwa mwaka 2010 ni tani za metriki 608,260 za wanga na tani za metriki 60,820 za mikunde. Hadi mwisho wa Septemba 2009 wilaya zote ziliripoti kwamba katika maeneo mengi chakula kilikuwa kinapatikana kwa kiwango cha wastani, japokuwa kuna maeneo machache ambayo yalikuwa na upungufu.
Inatarajiwa kwamba katika msimu wa kilimo 2009/2010 mkoa wa Kagera utaweza kujitosheleza kwa chakula, japokuwa ziada kwa ajili ya kuuza itakuwa ndogo. Hali ya upungufu mkubwa wa chakula inaweza kujitokeza katika maeneo kadha kama mvua za Vuli hazitaendelea hadi mwisho wa Desemba 2009
Malengo ya Ununuzi wa Mazao Msimu 2009/2010
Kahawa Maganda
Katika msimu wa ununuzi 2009/2010 makisio ya ununuzi wa kahawa kwa mkoa mzima wa Kagera ni tani 34,015 kwa wastani wa TSh 450/= kwa Kilogramu. Kiasi hiki ni kidogo ukilinganisha na msimu wa ununuzi 2008/2009, kwa sababu mvua zilinyesha mfululizo katika kipindi cha kutunga maua na hivyo maua mengi yalioza. Hadi 15 Oktoba Kilogramu 19,005,270 zenye thamani ya TShs 8,552,371,500.00 zilikwishanunuliwa.
Pamba Mbegu
Katika msimu wa 2009/2010 makisio ya ununuzi wa pamba mbegu ni tani11,800, kwa bei ya sasa ya TSh 440/= kwa kilogramu. Hadi 15 Oktoba 2009, Kilogramu 4,092,730 zenye thamani ya TShs 1,800,801,200.00 zilikwishanunuliwa.
Majani Chai
Katika msimu wa 2009/2010 makisio ya ununuzi ni tani 3,500 kwa bei ya sasa ya TSh 110/= kwa kilogramu. Msimu mpya wa ununuzi wa majani chai umeanza 01 Oktoba 2009.
Tumbaku
Katika msimu wa 2009/2010 makisio ya ununuzi ni tani 200 kwa bei ya sasa ya TSh 2,640/= kwa kilogramu. Msimu wa ununuzi wa tumbaku utaanza Aprili 2010.
MPANGO WA HALMASHAURI WA KUNUNUA MATREKTA YA MKONO (Power Tillers).
Agizo la Waziri Mkuu kuhusu kila Halmashauri ya Wilaya kujiwekea utaratibu wa kununua Power Tillers 50 na Power Tillers 20 kwa kila Manispaa kila mwaka, ulipokelewa wakati Halmashauri zimekwishakamilisha utaratibu wa kuandaa na kupitisha bajeti kwenye vikao vyote halali vya Hamashauri, na kuwasilisha bajeti hizo katika ngazi za juu kwa kuzingatia Ukomo wa Bajeti. Agizo hilo litaendelea kutekelezwa katika bajeti zijazo kama alivyoagiza Waziri Mkuu.
Katika bajeti ya mwaka 2009/2010 Halmashauri za Wilaya za Mkoa wa Kagera zimepanga kununua jumla ya matrekta ya mkono (Power Tillers) 97 kupitia Mipango ya Kuendeleza Kilimo Wilayani (DADPs), kwa gharama ya TShs 824,337,700 /= kwa mchanganuo ufuatao:
H/Wilaya Biharamulo – Matrekta ya Mkono 13 kwa gharama ya TSh 84,000,000.00
H/Wilaya Muleba – Matrekta ya Mkono 5 kwa gharama ya TSh 34,500,000.00
H/Wilaya Bukoba – Matrekta ya Mkono 15 kwa gharama ya TSh 120,000,000.00
H/Wilaya Karagwe – Matrekta ya Mkono 8 kwa gharama ya TSh 77,837,700.00
H/Manispaa Bukoba – Matrekta ya Mkono 0 kwa gharama ya TSh 0.00
H/Wilaya Chato – Matrekta ya Mkono 20 kwa gharama ya TSh 160,000,000.00
H/Wilaya Missenyi – Matrekta ya Mkono 6 kwa gharama ya TSh 48,000,000.00
H/Wilaya Ngara – Matrekta ya Mkono 30 kwa gharama ya TSh 300,000,000.00
MAAGIZO MAALUM YA SERIKALI KUHUSU KILIMO KWANZA
Baraza la Taifa la Biashara (TNBC), chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lilifanya mkutano tarehe 2 na 3 mwezi Juni 2009 jijini Dar es Salaam, kujadili sera na mikakati ya kuleta mapinduzi ya kilimo cha Tanzania pamoja na utekelezaji wake chini ya kaulimbiu ya “ KILIMO KWANZA ”
Kwa kutambua kuwa changamoto kubwa kwa Tanzania ni kupambana na umaskini na kwamba hili litawezekana hasa kwa kuongeza tija katika kilimo, mkutano huo uliazimia na kuagiza yafuatayo:
KILIMO KWANZA iwe ndiyo dhana ya kuleta mapinduzi ya kijani kwa lengo la kukifanya kilimo cha Tanzania kuwa cha kisasa na cha kibiashara;
Dhana ya KILIMO KWANZA ijumuishwe kwenye mipango mbalimbali ya Serikali ili kuhakikisha mafanikio ya utekelezaji wake;
Jitihada zifanyike katika kuongeza rasilimali mbalimbali ili kufanikisha utekelezaji wa KILIMO KWANZA ;
Sekta binafsi ihamasishwe ili iongeze uwekezaji kulingana na wajibu wake katika utekelezaji wa KILIMO KWANZA ; na
Utekelezaji wa KILIMO KWANZA utaongozwa na nguzo kumi zifuatazo:
I. Utashi wa kisiasa kutoa msukumo wa mapinduzi ya Kilimo.
II. Kugharamia mapinduzi ya Kilimo
III. Uboreshaji wa mfumo wa utawala wa kilimo.
IV. Mabadiliko ya mfumo mkakati katika kilimo.
V. Upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya kilimo.
VI. Vivutio vya kuchochea uwekezaji katika kilimo.
VII. Uendelezaji wa viwanda katika kuleta mapinduzi ya kilimo.
VIII. Sayansi, Teknolojia na Rasilimali Watu katika kuwezesha mapinduzi ya kilimo.
IX. Uendelezaji wa Miundombinu ili kuwezesha mapinduzi ya kilimo.
X. Uhamasishaji na ushirikishwaji wa Watanzania kuunga mkono na kutekeleza KILIMO KWANZA .
Maelezo kamilifu ya nguzo hizi kumi yaliyofafanuliwa katika programu ya kitaifa yamekwishatolewa. Mkoa umetekeleza hatua ya kwanza ya programu za Kitaifa kwa kuitisha mkutano wa wadau tarehe 22-23 Desemba, 2009, ambao ulipitia na kujadili nguzo zote za KILIMO KWANZA na hatimaye kuweka mikakati na mbinu za utekelezaji wa kila jukumu la kutekeleza shughuli za KILIMO KWANZA.
Baada ya mkutano huo, kila Wilaya/Halmashauri ilielekezwa kupitia upya maazimio ya mkutano na kutengeneza upya mpangomkakati wa kutekeleza KILIMO KWANZA unaoonesha vipaumbele vya Wilaya na viashiria vya kupima utekelezaji wa kila mkakati.
|