Kikao cha Bodi ya Barabara kimefanyika Mkoani Kagera na kubainisha changamoto mbalimbali zinazoikabili miundombinu ya barabara katika Mkoa wa Kagera pamoja na utatuzi wake. Aidha pamoja na changamoto zilizopo lakini barabara za Mkoa na Halmashauri za Wilaya Mkoa wa Kagera zinaridhisha na zinapitika kwa muda wote.
Kikao hicho kilifanyika tarehe 12/03/2011 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera na kuongozwa na Mhe. Mohammed A. Babu Mkuu wa Mkoa wa Kagera na Mwenyekiti wa kikao hicho. Mhe. Babu katika ufunguzi aliwapongeza wajumbe wa kikao kwa kuendelea kutunza barabara zote za Mkoa wa Kagera na kupitika kwa kipindi chote kwa mwaka mzima .
Pia Mhe. Babu aliwajulisha wajumbe wapya wa kikao hicho ambao ni Waheshimiwa Wabunge kuwa Bodi ya Barabara ya Mkoa si Bodi ya Utendaji yaani “Executive Board” bali ni Bodi ya Ushauri ambayo majukumu makubwa ni kujadili na kutoa ushauri kwa Waziri wa Ujenzi ambaye ndiye mwenye dhamana ya ujenzi, matengenezo na utunzaji wa barabara na madaraja ili kuleta tija na thamani halisi ya fedha inayotolewa na jinsi inavyotumika.
Changamoto ambayo imejitokeza kuanzia mwishoni mwa mwaka jana 2010 ni kusuasua na kupelekea kusimama kwa miradi mikubwa ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ya Kagoma – Lusahunga (km 154); Ushirombo – Lusahunga (km 110) na Kyaka – Bugene (km 59) kutokana na madeni ya malipo ya kazi ambazo tayari zimekwisha kukaguliwa na kuthaminiwa. Pamoja na changamoto hiyo Mhe. Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliwahakikishia wananchi wa Mkoa wa Kagera alipokuwa anafanya majumuisho ya ziara yake Mkoani Kagera kuwa fedha tayari zimelipwa na ujenzi wa barabara utaendelea mara moja.
Pia barabara zilizopandishwa hadhi/daraja ambazo ni Kyaka – Bugene – Kasulo (km 178); Omugakorongo – Kigarama – Murongo (km 106); Rutenge – Rubale – Izimbya – Omubweya – Buhamila – kishoju – (km 71) pia na Mukungo – Nyabusozi – Kabunda – Nyantakara (km 85.23) zimeendelea kupata matengenezo ya aina mbalimbali tangu zianze kuhudumiwa na Wakala wa Barabara. “Serikali inaendelea kutafuta vyanzo vingine vya fedha badala ya kutegemea mfuko wa barabara (Road Fund) pekee kama ilivyo sasa ili barabara zote zijengwe.” Alisema Mhe. Babu.
|