Aina za ufugaji
Aina mbalimbali za ufugaji zinaweza kutofautishwa katika wilaya ya Muleba. Aina kuu mbili ni ufugaji wa ng'ombe wa kienyeji ambao ndio ulioenea zaidi na wa pili ni ufugaji wa ng'ombe wa maziwa.
Ufugaji wa ng'ombe wa kienyeji
Ufugaji wa kawaida
Ufugaji huu hasa hasa ni kwa ajili ya kuzalisha mbolea ya kuweka kwenye migomba na mibuni. Suala la maziwa, nyama na ngozi si vya msingi, machungo yanakuwa ya zamu katika mbuga za wazi.
Ng'ombe wafugwao ni aina ya Zebu ambao huwa wana pembe fupi na kwa kiasi fulani Ankole. Usiku ng'ombe hufungiwa kwenye banda lililoezekwa lililo katikati ya shamba (kibanja)
Katika maeneo yenye watu wengi malisho huwa ni tatizo wakati wa kiangazi, ardhi kwa ajili ya kulima na kufuga huwa ni adimu. Maji ya kunyweshea mifugo si tatizo la msingi. Wanaume na vijana wa kiume ndio huwa wachunga ng'ombe. Ufugaji wa aina hii upo tarafa ya Kamachumu, Izigo na Muleba na kwa kiwango kidogo tarafa ya Kimwani na Nshamba.
Ufugaji wa kuhamahama
Uzalishaji wa mazao ya mifugo ndio shughuli kuu ya ki-uchumi. Wafugaji hawa huwa wanafuga idadi kubwa ya ng'ombe.
Ng'ombe wafugwao ni Ankole ambao kwa kawaida wana pembe ndefu.
Wafugaji hawa huwa hawana makazi ya kudumu kwani mara nyingi wanahamahama kutafuta malisho na maji hasa wakati wa kiangazi. Mifugo hutumika kama ishara ya utajiri na machungo hufanywa na familia nzima.
Katika mfumo huu wa ufugaji, uzalishaji wa mazao ya mifugo unapewa kipaumbele zaidi kuliko mfumo wa kwanza unaojali uzalishaji wa mbolea kwa ajili ya kilimo tu na si vinginevyo.
Mfumo huo unathamini mifugo kama akiba ya benki na hutumika kama dhamana. Ufugaji huu unapatikana katika maeneo machache ya Tarafa ya Muleba, Nshamba na Kimwani.
Idadi ya mifugo kwa kaya ni mingi ikilinganishwa na mfumo wa kwanza. Huandaa vibanda vya muda kwa ajili ya mifugo na huhamahama kutafuta malisho na maji wakati wa kiangazi.
Ufugaji wa n'gombe wa maziwa
Takribani kaya 2000 zinafuga ng'ombe wa maziwa wapatao 3,000 katika wilaya ya Muleba. Ng'ombe hawa hufugwa karibu na makazi (Zero grazing system) na zao kuu huwa ni maziwa, na mbolea hutumiwa mashambani.
Maziwa huuzwa hivyo kuwaongezea wakulima kipato. Kulingana na gharama za matunzo ng'ombe hawa hufugwa mara nyingi na wakulima wenye uwezo.
Mazao ya Mifugo
Januari 2008 ilifanyika sensa ya mifugo ilionyesha kuwa kaya 6934 zinafuga ng'ombe katika wilaya ya Muleba. Pia jumla ya kaya 23,514 zinafuga mifugo ya aina mbalimbali ambazo ni sawa na asilimia 42 ya kaya zote wilayani.Wilaya inajumla ya ng'ombe wa asili 82911, Ng'ombe wa maziwa 4464, Mbuzi wa maziwa 5449, Mbuzi asili 94954.
|