Inakadiriwa kuwa mwaka 2008 idadi ya wakazi wa mkoa wa Kagera imefikia 2,453,406 (maoteo). Mahitaji ya chakula kwa wakazi wa mkoa huu kwa mwaka 2008/09 ni tani za metriki 651,400 za wanga na tani za metriki 65,140 za mikunde.
Hadi mwisho wa Oktoba 2008 Wilaya zote ziliripoti kwamba chakula kilikuwa kinapatikana kwa kiwango cha wastani. Inatarajiwa kwamba katika msimu wa kilimo 2008/2009 mkoa utaweza kujitosheleza kwa chakula, endapo mvua zitanyesha kwa kiwango cha kawaida kama ilivyotabiriwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania. Maandalizi ya Ununuzi wa Mazao ya Biashara 2008/09
Kwa kawaida ununuzi wa mazao mkoani hutegemea sana vyama vya vikuu vya ushirika ambavyo ni Kagera Cooperative Union (KCU), Karagwe Cooperative Union (KDCU), Biharamulo Cooperative Union (BCU) na Ngara Farmers Cooperative Society. Aidha ununuzi unafanywa na makampuni na vikundi vya watu binafsi.
Katika msimu wa ununuzi 2008/09 Vyama Vikuu vya Ushirika viwili na kikundi kimoja cha wakulima wanajishughulisha na ununuzi wa mazao katika wilaya mbalimbali. Aidha makampuni tisa ya binafsi yameruhusiwa kununua kahawa katika wilaya za Bukoba, Missenyi, Muleba, Ngara na Karagwe. Makampuni sita ya binafsi yameruhusiwa kununua pamba wilayani Biharamulo na Chato. Ununuzi wa zao la tumbaku utaanza mwezi Aprili 2009; na Tanzania Leaf Tobacco Company (TLTC) yenye makao yake mjini Kahama.
Ununuzi wa Mazao ya Biashara Hadi Oktoba 2008
Mwanzoni mwa msimu wa ununuzi 2008/2009 bei za Kahawa m aganda kwa wanunuzi walio wengi walianzia kwenye wastani wa TShs 800/= kwa kilogramu. Kwa wanunuzi wa zao la pamba bei ya wastani ilikuwa ni TSh 400/= kwa kilo.
Hadi 31 Oktoba 2008 jumla ya tani 48,038 za Kahawa maganda zenye thamani ya Tshs. 37,407,451,120/= zilikuwa zimenunuliwa mkoani kote. Aidha hadi 31 Oktoba 2008 Pamba mbegu Tani 6,500 zenye thamani ya TSh 2,600,000,000/= zilinunuliwa.
Changamoto
Sekta ya kilimo mkoani Kagera inakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo ni pamoja na:
Magonjwa hatari ya mimea ambayo ni mnyauko bakteria wa migomba (Banana Xanthomonas Wilt), mnyauko fuzari wa kahawa (Coffee Fusarium Wilt), ugonjwa wa michirizi ya kahawia (Cassava Brown Streak Disease) na batobato kali ya mhogo (Cassava Mosaic Disease – UgVariant).
Idadi ndogo ya Maafisa Ugani isiyokidhi mahitaji. Hadi Oktoba 2008 Mkoa ulikuwa na jumla ya Maafisa Ugani 148 katika Halmashauri zake na kati ya hao 123 wako katika ngazi za Kata na Vijiji.
Vijana wengi wanaoishi vijijini wanashughulika na biashara ndogondogo badala ya kushiriki katika kilimo na wengine wanahamia mijini na hivyo kupunguza nguvukazi vijijini.
Wakulima kutumia pembejeo za viwandani kwa kiwango kidogo.
Kushuka kwa bei ya kahawa katika soko la dunia ambako kumesababisha bei ya Kahawa ishuke pia Mkoani.
Mikakati ya Kuendeleza Kilimo
Katika kupambana na changamoto zilizotajwa hapo juu Mkoa umeweka mikakati mbalimbali ya kuongeza uzalishaji wa mifugo na kilimo. Mikakati hiyo ni pamoja na:-
Kutumia sheria ndogo zilizopo katika Halmashauri za wilaya kuwabana na kuwawajibisha vijana wavivu.
Viongozi kuwajibika kwa kuyafanya mashamba yao kuwa ya mifano ya kilimo bora chenye tija.
Kuhimiza kilimo cha wanyamakazi zaidi kwenye maeneo yanayofaa kwa kilimo hicho hususan wilaya za Chato, Biharamulo na Missenyi.
Kuendeleza shamba la Kikulula la uzalishaji wa punda ambalo kwa sasa lina punda 130.
Kusimamia ufufuaji wa mashamba ya mazao ya biashara yaliyotelekezwa katika kila Halmashauri.
Kila Mtaalam wa Ugani kuwa na mpangokazi wa mwaka mzima kwa kutumia Daftari la Bwanashamba ili kuongeza uwajibikaji.
Kutumia kikamilifu mbegu bora za muhogo zinazozalishwa kwenye mashamba ya mbegu yaliyopo mkoani. Zipo jumla ya hekta 90 za mashamba mama ya kuzalisha mbegu ya mihogo inayovumilia batobato kali, zenye uwezo wa kuzalisha pingili milioni 27 kwa mwaka.
Kuhimiza na kuongeza matumizi ya aina mpya za migomba inayovumilia mashambulizi ya wadudu, migomba inayozalishwa katika mashamba ya Kyakailabwa, Nshambya na ARDI Maruku (Bukoba); Nkwenda (Karagwe) na Muleba. Aina hizi ni FHIA 17, FHIA 23, FHIA 25 na Yangambi Km5.
Kuzalisha miche bora ya kahawa kwenye bustani mama mbili za Ibwera (Bukoba) na Biirabo (Muleba) zenye uwezo wa kutoa jumla ya miche 720,000 aina ya kolona kwa mwaka. Aidha kila Halmashauri ya wilaya imeanza kuanzisha bustani za miche itokanayo na mbegu katika maeneo yanayofaa.
Halmashauri kwa kushirikiana na TaCRI na Vyama Vikuu vya Ushirika zitaendelea kununua mbegu bora za mazao na kuzisambaza kwa wakulima.
Kuunda “task forces” katika kila kijiji chenye ugonjwa wa Mnyauko bakteri wa migomba ili kuhakikisha ung'oaji wa migomba iliyougua unakamilika katika kipindi kifupi.
Kuhimiza vyama vikuu kuendelea kununua Kahawa na kutoa hamasa kwa wananchi kuendelea kutunza zao la kahawa, hata baada ya bei kushuka.
|