UKUZAJI VIUMBE HAI WA MAJINI
Ukuzaji wa viumbe hai kwenye maji umejikita zaidi kwenye ufugaji wa samaki tu; hii ni kutokana na hali halisi ya Mkoa kuzungukwa na maji baridi. Sambamba na hali hiyo mazingira ya ufugaji wa samaki yanaruhusu, kwani kuna rutuba nzuri na uwepo wa maji kwa muda wote wa mwaka. Samaki wanaofaa kufugwa katika mabwawa kulingana na jiografia ya Mkoa ilivyo ni pamoja na samaki aina ya Tilapia na Clarius.
Hata hivyo jamii kubwa ya watu wa Mkoa wa Kagera wana mwitikio mdogo wa ufugaji wa samaki kuliko ufugaji mwingine wowote wa viumbe hai wa majini.
Takwimu zinaonesha kuwa Mkoa ulikuwa na mabwawa 360 mwaka 2007; mabwawa mengi yaliyokuwa yameanzishwa kipindi cha nyuma hayafanyi kazi kwa sasa, hii inatokana na kutokuwa na vifaranga bora vya samaki, na elimu duni juu ya uchimbaji na utunzaji wa mabwawa hayo kwa wakati huo.
Hivi sasa kuna uingizaji haramu wa samaki hai wanaotumika kama chambo katika uvuvi wa sangara aina ya kambale ( Clarius gariepinus ) ndani ya nchi yetu wakitokea nchi jirani ya Rwanda, Uganda na Burundi. Hii ni biashara inayowaingizia wadau fedha nyingi hivyo kufanya dhana ya utumiaji wa mabwawa yaliyochimbwa kupungua. Aidha ni hatari kwa suala la uingizaji wa magonjwa na pia kuua mbegu ya samaki wa asili wa nchi hii. Kambale hawa hutumiwa na wavuvi wa Sangara kama chambo (live bait)
MAFANIKIO KATIKA SEKTA YA VIUMBE HAI MAJINI.
Katika kipindi cha Oktoba 2008 hadi Novemba 2009 ufuatiliaji ulifanyika katika Halmashauri 7 na kubainisha yafuatayo
- Kuwepo kwa mabwawa 197 na wafugaji 1,341 ambao wameelimishwa juu ya ufugaji samaki,
- Kupandikizwa Idadi ya vifaranga 37,423 aina ya sato (rejea Jedwali Na.5), na samaki waliovunwa ni Kilogramu 5,500 aina ya Sato ambao walikuwa na thamani ya Tsh 1,100,000/=.
- kutolewa kwa vibali 8 vya kusafirisha vifaranga kwa kipindi hicho. Hii inatokana na mwamko mdogo wa wananchi katika kuelewa umuhimu wa kutumia vibali. Hata hivyo elimu itaendelea kutolewa kwa wananchi juu ya umuhimu wa kufuata utaratibu.
Kuchimba bwawa la mfano lenye ukubwa wa mita 10 kwa 10 katika Manispaa ya Bukoba, eneo la ofisi ya Doria Mkoa ambalo linatarajiwa kupandikizwa samaki aina ya Tilapia wapatao 20,000 katika kipindi cha mwaka 2009/2010. Bwawa hilo pia linatarajia kuwa la mfano kwa kuelimisha wafugaji na kutoa vifaranga kwa wafugaji wa samaki kimkoa
MIKAKATI YA KUENDELEZA NA KUSIMAMIA RASILIMALI YA UVUVI
Mkoa umejiwekea mikakati mbalimbali ya kuendeleza Sekta ya Uvuvi pamoja na udhibiti wa uvuvi haramu na uharibifu wa mazingira. Juhudi hizi zinafanywa kwa kuzingatia sheria ya uvuvi na kanuni zake.Mkoa utahakikisha panakuwepo utashi wa kisiasa katika ngazi zote ili kutekeleza Yafuatayo;
kuandaa mipango ya kila Halmashauri ya kudhibiti ongezeko la nguvu ya uvuvi kwa kutoa kiwango fulani cha idadi ya leseni ili kutunza rasilimali ya uvuvi.
Kuweka mikakati ya nyongeza ya ajira kwa maafisa ugani katika Halmashauri zote ili kuongeza idadi kutoka 26 walioko sasa hadi kufikia 56 ili kujaza mapengo yaliyopo katika upungufu wa maafisa ugani katika Halmashauri.
Kuendelea kutoa elimu ya madhara ya maambukizi ya ukimwi kwa wavuvi katika mialo,
Kuhakikisha Halmashauri zinashirikiana na BMU's kulinda rasilimali za uvuvi na ukusanyaji mapato yatokanayo na sekta ya uvuvi,
Kuhakikisha NGO's zinaendeleza juhudi za dhati kwa kutoa elimu, mikopo na uibuaji wa miradi mbadala ili kupunguza nguvu ya uvuvi na uvuvi haramu katika ziwa Victoria .
kuratibu ubainishaji wa wajasiriamali katika sekta ya uvuvi kwa kuwapa elimu ya ufugaji wa samaki katika Wilaya zote.
Kutoa msaada vijijini wa kuibua miradi ya ufugaji viumbe hai (samaki) ili miradi hiyo iingizwe kwenye Mipango ya Halmashauri ya Kuendeleza Kilimo na ufugaji (DADPS na DASIP).
Kushirikisha vyombo vyote vya ulinzi na usalama katika kudhibiti wafanyabiashara wasiofuata sheria za uvuvi na kanuni zake.
Kuhamasisha wananchi kuchimba mabwawa ya kufugia samaki katika Wilaya zote.
|